BEKI wa zamani wa Yanga, Abdallah Shaibu 'Ninja' amefichua juu ya dili la kujiunga na FC Tanganyika inayoshiriki Ligi Kuu ya DRC Congo.
Mwanzoni mwa mwaka huu Ninja alithibitisha yupo kwenye mazungumzo na klabu hiyo ikiwa ni wiki chache tangu aachane na FC Lupopo.
Ninja alijiunga na Lupopo msimu uliopita akitokea Lubumbashi Sports ya nchini humo aliyoichezea kwa msimu mmoja kati ya miwili aliyokuwa amesaini na sababu ya kuachana nayo ni changamoto ya mshahara.
Akizungumza na Mwanaspoti, Ninja alisema mambo hayajakwenda kama alivyotarajia na tangu wakati ule uongozi wa timu hiyo haujamfuata kuendelea na mazungumzo.
"Nahisi wana mambo mengi, mwanzoni tulizungumza lakini sijajua tena wenyewe lakini kwa sasa nipo nchini naendelea na mazoezi ili kujiweka fiti kwa lolote," alisema Ninja
"Bongo kuna timu zimenifuata pia, lakini kwa sasa siwezi kuzungumza hadi pale tutakapokubaliana na kufikia muafaka ila kwa ofa zipo ndani na nje."