Viwanja vitano kufanyiwa ukarabati kuelekea AFCON 2027

Serikali imethibitisha rasmi mpango wa kujenga na kukarabati viwanja mbalimbali vya michezo nchini, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuandaa mashindano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) mwaka 2027, pamoja na juhudi za kuendeleza sekta ya michezo nchini.

Kauli hiyo imetolewa leo bungeni jijini Dodoma na Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Damas Ndumbaro, alipokuwa akiongeza majibu ya serikali kuhusu mipango ya kufufua na kuimarisha miundombinu ya michezo nchini.
“Katika maandalizi ya AFCON 2027, serikali imetenga viwanja vitano kwa ajili ya ukarabati vitakavyotumika kwa mazoezi ya timu shiriki. Viwanja hivyo ni Jamhuri (Morogoro), Mkwakwani (Tanga), Sokoine (Mbeya), CCM Kirumba (Mwanza), pamoja na Majimaji (Songea),” amesema Dk Ndumbaro.

Awali, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Profesa Palamagamba Kabudi, alijibu swali la Mbunge wa Songwe Mjini, Philipo Mulogo kuhusu ukosefu wa uwanja wa michezo katika mkoa huo na kueleza kuwa tayari serikali imeanza mchakato wa awali wa kujenga viwanja vipya katika mikoa mbalimbali.

“Natambua hali ya Uwanja wa Sokoine, lakini mahitaji ya viwanja ni makubwa nchini kote. Tayari katika bajeti iliyopitishwa, tunaanza upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujenga viwanja vingine 26 katika maeneo mbalimbali ya Tanzania. Ninaamini Mkoa wa Songwe utakuwa miongoni mwa maeneo yatakayokidhi vigezo hivyo,” amesema Profesa Kabudi.

Imeandikwa na

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *