TMA yatahadharisha uwepo wa mvua ya mawe, upepo na radi

Mbeya. Mamlaka ya Hali ya Hewa  (TMA) Kanda ya Nyanda za Juu Kusini  imewataka  wavuvi wa Ziwa Nyasa Wilaya ya Kyela mkoani hapa kuchukua tahadhari kufuatia kuwepo kwa  mvua ya mawe itakayoambatana na upepo mkali, mawimbi na  wingu la radi.

Pia, wavuvi hao wametakiwa kuepuka  kasumba  ya kutumia njia za jadi kutabiri athari za  majini kwa ajili ya kuendelea na shughuli za uvuvi.

Meneja wa Mamlaka ya Hali ya Hewa (TMA) Kanda, Elias Lipiki ameliambia Mwananchi Digital leo Jumatano Februari 12, 2025 alipohojiwa kuhusiana na utabiri wa athari za shughuli za uvuvi katika Ziwa Nyasa.

“Awali  mvua   zilichelewa  kunyesha  zilianza  mwishoni mwa mwezi  Desemba, 2024 na  zinatarajiwa  kuisha mwanzoni kwa mwezi Mei, 2025 katika maeneo ya maziwa kutakuwa na dhoruba itakayo sababisha wingu kubwa la radi, upepo mkali na mawimbi yenye uwezo mkubwa wa kupindua vyombo vya majini na  kusababisha madhara  kwa wavuvi,” amesema.

Lipiki  amesema ili kukabiliana na hali hiyo  umefika wakati  wavuvi kutopuuza utabiri wa hali ya hewa, licha ya kuwa na mifumo yao binafsi ya kutumia ujuzi  wa njia za jadi ambazo sio salama kwao.

“Kipindi hiki ni hatari sana kwa wavuvi kuingia majini kufuatia kuwepo na upepo mkali unao ambatana na  mawimbi makubwa, wingu la radi hali ambayo inaweza kuleta athari ya kuzama  mitumbwi, vifo, majeruhi na nyumba kuezuliwa,” amesema.

Amesema vipindi vya dhoruba  majini utokea kuanzia majira ya  alfajiri kunapoanza kukucha  mpaka saa  tisa alasiri  na kudumu kwa muda wa  nusu saa majini.

Ametaja sababu ya kutokea hali hiyo ni kutokana na uwepo wa wingu la radi katika maeneo ya maziwa hususani kwa Ziwa Nyasa Mkoa wa Mbeya.

Kuhusu athari kwenye uzalishaji, Elias amesema  wakulima  watumie fursa ya uwepo wa mvua hizi kuendelea kuzalisha kutokana na udongo kuwa na wingi wa maji ya kutosha.

“Changamoto ipo kwa upande wa utekelezaji wa miradi hususani  ya ujenzi wa barabara na vinginevyo wakandarasi  wachukue tahadhari kubwa katika kipindi hiki ambacho siyo rafiki  kuweza kukamilisha kufuatia uwepo wa mvua nyingi  zinazo tarajiwa kuisha mwanzoni mwa mwezi Mei mwaka huu,” amesema.

Wakati huo huo amesema utabiri umeonyesha  kipindi cha wiki mbili sasa mito imeanza kujaa maji na kuhatarisha wananchi  wanaoishi mabondeni.

“Maeneo mengi ya mito imeonyesha ongezeko la maji na kuna uwezekano wa  kina  kuongezeka kufuatia mvua zinazo endelea kunyesha  ni vyema wananchi wa maeneo ya mabondeni kuchukua tahadhari,” amesema.

Amesema kufuatia hali hiyo,  TMA wako kwenye mikakati ya kutumia mfumo wa utoaji taarifa za  hali ya hewa  kupitia mitandao ya simu za mkononi  kwa wavuvi na wananchi ili wachukue  tahadhari mapema.