
Polisi jijini Dar es Salaam Tanzania wamezingira jengo la kanisa la Ufufuo na Uzima linalomilikiwa na mbunge wa jimbo la Kawe Josephat Gwajima, ambaye wiki iliyopita, alilaani matukio ya utekaji nchini humo.
Imechapishwa: Imehaririwa:
Dakika 1 Wakati wa kusoma
Matangazo ya kibiashara
Hatua hiyo ilikuja saa chache baada ya kusambaa mtandaoni barua kutoka moja ya idara za Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ya Tanzania ikimuarifu Gwajima kuhusu uamuzi wa serikali kulifunga kanisa hilo.
Taarifa za askari polisi kulizingira jengo la kanisa la Ufufuo na Uzima lililopo eneo la Ubungo, kilomita 12 kutoka katikati mwa Dar es Salaam zilisambazwa mtandaoni na Gwajima mwenyewe kupitia kipande cha picha ya video akiwa amezungukwa na watu aliowaita maaskofu wa kanisa hilo waliovalia makoti na mashati ya rangi ya zambarau.
Baadaye zilisambaa picha zilizowaonesha watu wakirusha mawe na sauti za kuwahimiza waumini kwenda kanisani huku kukiwa na milio ambayo haikufahamika iwapo ilikuwa ni ya gesi ya kutoa machozi au risasi za moto.
Barua ya msajili wa jumuiya za kiraia iliyosambaa ambayo Gwajima anasema hajaipookea, ilielezea kufuta usajili wa kanisa la Glory of Christ Church maarufu Ufufuo na Uzima hivyo kutakiwa kusitisha shughuli zote mara moja kwa makosa ya kutoa mahubiri yanye mwelekeo wa kisiasa na kuichonganisha serikali na wananchi.
Mapema Mei 25 Gwajima alielezea kukerwa na matendo ya utekaji wa watu na mauaji.