RPC Mbeya aonya uvunjifu wa amani kuelekea uchaguzi mkuu, awapa neno vijana

Mbeya. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limewataka vijana kutumia michezo kama sehemu ya kuhamasisha amani na utulivu katika kuelekea uchaguzi Mkuu Oktoba 2025, huku likionya wavunjifu wa amani.

Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Benjamin Kuzaga amesema leo Jumamosi Mei 3, 2025, katika viwanja vya Kumbukumbu ya Sokoine baada ya kushiriki mbio za pole ikiwa ni kuelekea mashindano ya mbio “Betika Tulia Marathon 2025”, zinazotarajiwa kufanyika  Mei 9 mpaka 10 mwaka huu.

Amesema katika kuelekea uchaguzi mkuu Oktoba 2025, Serikali inahimiza wananchi kushiriki kikamilifu na kuachana na vitendo vya uvunjifu wa amani ambavyo havita vumilika.

“Tunaelekea  uchaguzi mkuu  jamii inapaswa  kushirikiana kikamilifu na Serikali  kutumia  kama sehemu ya  kulinda amani na sio vurugu ambazo hazitavumilika,”amesema Kuzaga.

Katika hatua nyingine, amewataka vijana kuchangamkia fursa ya  kushiriki mashindano ya mbio  za  “Betika Tulia Marathon 2025”   kwa lengo la kujenga umoja na mshikamano na kuibua vipaji kutoka Mkoa wa Mbeya.

“Itakuwa aibu sana kwa wananchi wa Mbeya kushindwa kushiriki, badala yake watu kutoka mataifa mengine kuibuka washindi kwa kujinyakulia zawadi,”amesema.

Mratibu wa mashindano hayo, Joyce Mwakifwamba amesema huu ni msimu wa tisa ambao umekuja  kitofauti kwa kuongeza  mbio za  kilometa mbili mpaka  tano ambazo zitahusisha watoto, huku watu wazima watakimbia kuanzia   mita 100 mpaka kilometa 42 .

“Lengo la kushirikisha watoto katika msimu huu ni kuibua vipaji na kuviendeleza kama njia pekee ya kujiajiri,”amesema.

Meneja wa Taasisi ya Tulia Trust ambao ni waandaji  wa mashindano ya mbio hizo, Jackline Boaz amesema leo Jumamosi  Mei 3, 2025 wameanza na mbio za awali kwa kushirikisha  wadau mbalimbali vikiwepo vyombo vya ulinzi na usalama  ambao wamekimbia umbali wa  kilometa 10.

“Huu ni mwanzo wa kuelekea mashindano ya mbio hizo ambazo zitashirikisha mataifa mbalimbali ya nje ya Tanzania ikiwepo  nchi jirani  ya Kenya,” amesema.

Boaz amehamasisha wananchi na wanariadha kujisajili wakiwepo wakazi wa Mbeya kwa kuzingatia riadha ni sehemu ya ajira na kujiajiri.

Ofisa Uhusiano wa Taasisi ya Tulia Trust, Joshua Mwakanolo amesema fedha za ushiriki kwenye mashindano hayo uelekezwa kuchangia miradi ya elimu, afya na kuwezesha kaya zisizo jiweza kiuchumi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *