
Papa Francis amewasili Jumatano hii nchini Kenya, hatua ya kwanza ya ziara yake ya siku tano barani Afrika ambayo pia itampeleka Uganda na Jamhuri ya Afrika ya Kati.
Imechapishwa:
Matangazo ya kibiashara
Ndege ya iliyomsafirisha Kiongozi wa Kanisa Katoliki kwa hatua ya kwanza ya ziara yake barani Afrika imeegesha Jumatano mchana katika uwanja wa ndege wa Nairobi. Papa Francis ataadhimisha Misa katika Chuo Kikuu cha Nairobi Alhamisi hii, ambapo siku hiyo imetangazwa kuwa likizo ya kitaifa. Askari polisi elfu kumi wamewekwa katika maeneo mbalimbali kwa usalama wa Kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki duniani.
Katika hotuba aliyoitoa mara baada tu ya kuwasili kwake kwenye Ikulu, makazi rasmi ya Rais Uhuru Kenyatta, Papa amewataka viongozi wa dunia kulinda mazingira na kutetea maendeleo endelevu kwa kufikiria vizazi vijavyo. Papa Francis amepanda mti katika bustani ya makazi ya rais.
Papa Francis pia atazungumzia suala la tabia nchi Alhamisi wiki hii katika hotuba yake kwenye ofisi ya Umoja wa Mataifa mjini Nairobi.
Katika hotuba yake Ikulu, Papa Francis amewatolea wito “wanaume na wanawake wote wenye nia nzuri njema kujihusisha na masuala ya maridhiano, amani na msamaha” dhidi ya “mgawanyiko wa kikabila, kidini na kiuchumi.”
“Kipaumbele kwa sasa ni mazungumzo kati ya imani tofauti”, amesema kwa upande wake, Rais Kenyatta, Mkatoliki kama 30% ya wananchi wake.
Kenya na Uganda zilikumbwa katika miaka ya hivi karibunina mashambulizi ya makundi ya kiislamu, na nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, kumeendelea kushuhudiwa vita kati ya Wakristo na Waislamu.
“Nakwenda kwa furaha nchini Kenya, Uganda na kwa ndugu zetu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati. Nina imani kuwa safari hii itazaa matunda, ya kiroho na kimwili”, amesema Papa katika ndege iliyokua ikimsafirisha kwenda Kenya.
Kanisa Katoliki lina waumini milioni 200 barani Afrika kulingana na takwimu za mwaka 2012. Idadi hii inaweza kuwa maradufu na kufikia hadi milioni 500 mwaka 2050.