NSSF yajivunia kasi ya ufanisi na mafanikio katika sekta ya hifadhi ya jamii nchini

Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) umeanika mafani­kio lukuki ya ufanisi kiutendaji ambayo yamepatikana katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Awamu ya Sita wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Akizungumzia mafanikio hayo, Masha Mshomba, Mkuru­genzi Mkuu wa NSSF, anasema Mfuko unaendelea kusimamia vizuri shughuli za hifadhi ya jamii kwa kuifikia sekta binafsi na sekta ya waliojiajiri.

Katika kipindi cha miaka minne ya Uongozi wa Mhe. Dkt. Samia, Umma wa Watanza­nia umeendelea kupata elimu kuhusu umuhimu wa kujiwekea akiba kwa ajili ya maisha yao ya sasa na ya baadaye kwa kuji­unga na kuchangia NSSF.

Aidha, kwa niaba ya Bodi ya Wadhamini, Bw. Mshomba anasema NSSF wanaungana na Watanzania wote kumponge­za na kumshukuru Mhe. Dkt. Samia kwa mafanikio makubwa aliyoyapata katika kuongoza nchi ambapo sasa anatimiza miaka minne tokea alipoapish­wa kushika wadhifa huo.

“Napenda kutumia fursa hii kumpongeza Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta maendeleo kwa Watan­zania ambapo katika uongozi wake tunashuhudia akiendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miradi mikubwa ya kimkakati. Kwa upande wa NSSF, miradi hiyo imekuwa ni fursa kwetu kupata wanachama pamoja na kuku­sanya michango,” anasema Bw. Mshomba.

Kuhusu sekta ya hifadhi ya jamii kwa ujumla, Bw. Mshomba ameeleza kuwa Watanzania ni mashuhuda wa namna ambavyo Mhe. Rais Dkt. Samia ameisi­mamia vizuri na kuwa na ufani­si mkubwa katika kipindi amba­cho amekuwa madarakani.

NSSF inatekeleza maju­kumu makuu manne ya msingi ambayo ni kuandikisha wana­chama kwa mujibu wa Sheria ya NSSF, kukusanya michango, kuwekeza na kulipa mafao. Kwa mujibu wa sheria, wanaotaki­wa kuandikishwa kuwa wana­chama wa NSSF ni wafanyakazi walioajiriwa katika sekta bin­afsi, raia wa kigeni wanaofanya kazi Tanzania Bara, watumishi wa taasisi za kimataifa zinazo­fanya kazi Tanzania Bara na wananchi waliojiajiri.

Ongezeko la wanachama, uwekezaji na ukuaji wa mfuko

Akizungumzia mafanikio ya NSSF kwa upande wa uandiki­shaji wanachama, Mshomba anasema Mfuko unaende­lea kutambua na kuandikisha wanachama wapya katika sekta binafsi na sekta ya waliojiajiri, ambapo katika kipindi cha mia­ka minne (Machi, 2021 mpaka Februari, 2025) ya Serikali ya awamu ya sita, NSSF imeandiki­sha jumla ya wanachama wapya 1,052,176.

Kwa upande wa ukusanyaji michango, Mshomba anasema kutokana na juhudi mbalimbali za Serikali ya awamu ya sita kuvutia uwekezaji na kufungua fursa mpya za biashara pamoja na jitihada za NSSF kuboresha utendaji wake, Mfuko umeonge­za uwezo wake wa kukusanya michango ambapo jumla ya shi­lingi trilioni 6.99 zimekusanywa kutoka kwa wanachama.

Aidha, wastani wa maku­sanyo ya michango kwa mwezi yameongezeka kutoka trilioni 1.13 katika mwaka ulioishia mwezi Februari 2021 hadi kufikia trilioni 2.15 mwezi Feb­ruari 2025, sawa na ongezeko la asilimia 90.

Daraja la Kigamboni ni moja ya miradi iliyotekelezwa na NSSF.

Mshomba anasema katika kipindi cha miaka minne, tha­mani ya Mfuko imeongezeka kutoka shilingi trilioni 4.8 mwezi Februari 2021 na kufikia trilioni 9.2 mwezi Februari 2025, sawa na ongezeko la asil­imia 92.

Anasema, tathimini inaone­sha hali ya ustahimilivu wa Mfu­ko ni asilimia 90.7 kwa kipindi kilichoishia mwezi Juni 2023 ukilinganisha na asilimia 87.7 iliyokuwepo katika tathimini ya kipindi kilichoishia mwezi Juni 2020. Hali hii inaashiria uhai na uendelevu wa Mfuko. Aidha, Mfuko umeendelea kulipa kodi ya Serikali kwa mujibu wa she­ria na hivyo kuchangia katika kuiwezesha Serikali kutekeleza miradi mikubwa hapa nchini.

Mshomba anasema Mfuko umelipa kodi ya shilingi bilioni 380 ambayo ni sawa na wastani wa shilingi bilioni 75 kwa mwa­ka. Aidha, katika siku ya walipa kodi, Mfuko ulitunukiwa tuzo na Mamlaka ya Mapato Tanza­nia (TRA) ya mlipa kodi mzuri kwa hiari kitaifa kwa mwaka 2023/24.

Malipo ya mafao

Mshomba anasema katika kipindi cha miaka minne, Mfuko ulilipa mafao ya shilingi tril­ioni 3.10 na malipo ya mafao kwa mwaka yaliongezeka kwa asilimia 69 kutoka shilingi bil­ioni 537.08 katika mwaka ulio­ishia mwezi Februari 2021 hadi kufikia shilingi bilioni 909.16 mwezi Februari 2025.

Anasema katika mabadiliko ya kanuni ya ulipaji mafao ya kustaafu (KIKOKOTOO) yaliyo­fanyika na kuanza kutekelezwa mwezi Julai, 2022 wastaafu wa NSSF walianza kupokea mkupuo wa awali wa asilimia 33 ukilinganisha na asilimia 25 waliokuwa wakilipwa kabla ya mabadiliko hayo. Aidha, kuto­kana na Serikali ya awamu ya sita kuwajali wastaafu, Mfuko umeendelea kuboresha tena ulipaji wa mafao kwa wana­chama wote waliokuwa wan­alipwa mkupuo wa awali wa asilimia 33 na kufikia asilimia 35. Ongezeko hili lilifanyika kwa wastaafu wote waliostaafu kuanzia mwezi Julai, 2022.

“Uamuzi huu wa Serikali wa kuongeza kiwango cha malipo ya mkupuo kwa wanachama wa NSSF pia umezingatia uende­levu wa Mfuko,” anasema Bw. Mshomba.

Anasema Mfuko katika hatua za mwisho za kuboresha kiwan­go cha kima cha chini cha pen­sheni ya kila mwezi kwa wasta­afu kutoka shilingi 100,000 hadi shilingi 150,000. Viwango vingine vya pensheni vinatara­jiwa pia kuongezeka kwa kati ya asilimia 2 na asilimia 20.

Maboresho ya huduma na matumizi ya Tehama

Kuhusu maboresho ya huduma na matumizi ya TEHAMA, Mshomba anasema Mfuko umefanya maboresho mbalimbali katika utendaji ili kuwezesha wanachama kupata huduma mbalimbali kwa ura­hisi na kupunguza usumbufu, ambapo moja ya hatua hizo ni kuanzishwa kwa mikoa ya mipya ya huduma ya Ubungo na Kigamboni, Dar es Salaam pamoja na kupandishwa hadhi vituo vitatu vya Mkuranga, Hai na Mbezi Beach kuwa na hadhi ya ofisi za wilaya.

Bw. Mshomba anasema kwa kuzingatia matumizi ya TEHAMA ni moja ya maeneo yanayotiliwa mkazo na Seri­kali ya awamu ya sita, Mfuko umebainisha eneo hilo kuwa la kipaumbele ambapo baa­dhi ya maboresho ya mifumo yamewezesha waajiri na wana­chama wa NSSF kujihudumia na kupata huduma mbalimbali kupitia mifumo ya TEHAMA, pasipo kulazimika kufika katika ofisi za NSSF.

“Matumizi ya TEHAMA katika utendaji wa Mfuko yameongezeka kutoka asilimia 48 iliyokuwa imefikiwa mwezi Februari 2021, hadi kufikia asil­imia 87.5 mwezi Februari 2025, ikitarajiwa kufikia asilimia 100 ifikapo mwezi Juni 2025,” anas­ema Bw. Mshomba.

Mradi wa Mkulazi

Akizungumzia mradi wa kiwanda cha sukari Mkulazi, Mshomba anasema Mfuko kupi­tia kampuni tanzu ya Mkulazi, umekamilisha ujenzi wa kiwan­da hicho. “Kiwanda hiki kiliz­induliwa tarehe 7 Agosti 2024 na Rais wa Jamhuri ya Muun­gano wa Tanzania, Mhe, Dkt. Samia Suluhu Hassan baada ya uzalishaji wa sukari ya majum­bani kuanza rasmi mwezi Julai 2024,” anasema Bw. Mshomba.

Anasema hadi kufikia mwezi Februari 2025 tani 19,124 za sukari ya majumbani zilikuwa zimezalishwa na kupelekwa sokoni. Kiwanda kimetoa fur­sa za ajira 8,302 ambapo ajira za moja kwa moja ni 1,665 na zisizo za moja kwa moja ni 6,637. Matarajio ni kwenda kutoa fursa za ajira zaidi ya 11,315 ya baa­da ya uzalishaji sukari kufikia kiwango cha juu. Aidha, mradi huo pia unatarajiwa kuzalisha megawati 15 za umeme ambazo kati yake megawati 7 zinatarajiwa kuingizwa katika gridi ya Taifa kupitia kituo cha kupoke­lea na kupo­za umeme cha Msamvu Morogoro.

Kuwaon­dolea kero Wananchi wa Kigam­boni

Mshomba anasema Mfuko una­ishukuru Serikali ya awamu ya sita kwa kuwaondolea kero wananchi wa Kigamboni ambao walikuwa na malalamiko ya muda mrefu kuhusu viwango vya tozo wal­izokuwa wakilipa wanapovuka Daraja la Nyerere, Kigamboni.

Anasema kupitia uamuzi wa Serikali, viwango vya tozo vili­shushwa na kuanzisha malipo kwa utaratibu wa vifurushi (bundle) ambavyo vina unafuu mkubwa kwa watumiaji wa Daraja.

Bw. Mshomba anasema was­tani wa makusanyo ya mapato katika Daraja la Nyerere, yame­ongezeka kwa mwezi kutoka shilingi bilioni 1.13 mwezi Feb­ruari 2021 hadi kufikia shilingi bilioni 1.89 katika kipindi cha mwezi Februari 2025, sawa na ongezeko la asilimia 66.

Changamoto za miradi ya uwekezaji iliyokuwa imesi­mama zimetatuliwa

Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, Mshomba anasema Mfuko umetatua changa­moto zilizokuwa zinakabili miradi ya ujenzi na kusa­babisha miradi ya Dungu, Toan­goma, Kijichi III, Mzizima na Hoteli ya kitalii Mwanza kusimama kati ya mwaka 2016 na 2021 kupisha zoezi la ukaguzi maalumu. Anas­ema utatuzi ulio­fanyika unahusi­sha upatikanaji wa mwendesha hoteli kwa ajili ya miradi ya Mzizima na hoteli ya kitalii ya Mwanza pamoja na kutatua changa­moto za mikataba na wakandarasi waliokuwa wame­tekeleza miradi ya Dungu, Toangoma na Kijichi III.

“Kwa sasa miradi yote hii inaendelea na kutarajiwa kuka­milika kati ya Juni 2025 na Juni 2026,” anasema Bw. Mshomba.

Skimu ya Uchangiaji wa Hiari kwa Wananchi waliojiajiri

Mshomba anasema Mfuko unajivunia kutoa huduma za hifadhi ya jamii kwa wananchi walioajiriwa kwenye sekta bin­afsi na waliojiajiri kwa kuzinga­tia maelekezo ya Ilani ya Ucha­guzi ya CCM ya mwaka 2020- 2025 na Ibara ya 11 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayozungumzia umuhimu wa Watanzania kuji­unga na kunufaika na sekta ya hifadhi ya jamii, jukumu ambalo linatekelezwa vyema na NSSF.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu – Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Ridhiwani Kikwete akitoa elimu kwa wananchi waliojiajiri wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya “NSSF Staa wa Mchezo” Mbagala Zakhem, Dar es Salaam.

Anasema Mfuko unaende­lea na maboresho ya Skimu ya uchangiaji wa hiari kwa wananchi waliojiajiri (Hifa­dhi Scheme) ambapo kupitia mpango huo wananchi waliojia­jiri katika shughuli mbalimbali kama vile kilimo, ufugaji, uvuvi, uchimbaji mdogo wa madini, sekta ya usafirishaji (boda boda, bajaji) mama na baba lishe pamoja wajasiriamali wengine wote wataweza kupata huduma za hifadhi ya jamii kama wana­vyonufaika wanachama walioa­jiriwa katika sekta binafsi.

Anasema hadi kufikia mwezi Februari 2025, wanachama 437,319 wamejiunga kwenye skimu hiyo na wanaendelea kunufaika na mafao kama pen­sheni ya uzeeni, urithi, uzazi, matibabu, ulemavu na mafao ya kujitoa. Skimu ya Hifadhi (Hifa­dhi Scheme) inatarajiwa kuz­induliwa rasmi mwezi Aprili, 2025.

Mshomba anasema tayari Mfuko umezindua kampeni ya “NSSF Staa wa Mchezo” amba­po ujio wa “Hifadhi Scheme” unatoa nafasi kwa NSSF kushika usukani na kuwa staa wa mche­zo katika maisha ya uzeeni au pindi majanga yanapotokea kwa wananchi waliojiajiri. Kuji­unga na kuchangia ni rahisi tu kwa kubofya *152*00# ambapo mwanachama anaweza kuchan­gia shilingi 30,000 au zaidi kwa kutoa kidogo kidogo kwa siku, wiki, mwezi au msimu kulinga­na na kipato chake na kunufaika na mafao yote yanayotolewa na NSSF yakiwemo ya matibabu.

Matarajio ya Mfuko kwa mujibu wa Mpango wa Maendeleo wa Muda Mrefu

Bw. Mshomba anaeleza kwamba matarajio ya Mfuko ni pamoja na;

• Kuendelea kutekeleza mikakati ya ukuaji wa Mfuko ili kuhakikisha kwamba thamani ya Mfuko inafikia zaidi ya shilingi trilioni 11 mwezi Juni 2026, ikiwa ni mara mbili ya thamani ya shi­lingi trilioni 5.078 iliyo­fikiwa mwezi Juni 2021.

• Kuendelea kubaini fursa za uwekezaji katika mae­neo mapya yenye faida zaidi na salama ikijumui­sha masoko ya hisa na mitaji katika Jumuiya ya Afrika Mashariki na SADC ili kuweza kuwa na mtawanyo mzuri wa vitega uchumi.

• Kuimarisha mifumo na matumizi ya TEHAMA ili kuongeza ufanisi, kupun­guza malalamiko kwa wateja na kutoa huduma bora kwa wanachama wake.

• Kuendelea kutekeleza Skimu ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii kwa Wananchi waliojia­jiri yaani “Hifadhi Scheme” ili kuvutia wananchi waliojiajiri kujiunga na huduma za Hifadhi ya Jamii ambapo watanufaika na huduma mbalimbali zinato­tolewa ikiwa ni pamoja na mafao ya matibabu.

Mshomba anahitimisha kwa kutambua mchango na ush­irikiano ambao Mfuko umepata kutoka kwa waajiri na wana­chama wetu kote nchini kama sehemu ya mafanikio anayoy­aeleza.

“Niishukuru tena Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ili­yofanyika katika kipindi hiki cha miaka minne (4) kwa kuweka mazingira mazuri na wezeshi ya uwekezaji na hivyo kuruhusu wawekezaji wengi nchini walio­changia kukuza ajira na kuon­geza idadi ya wanachama kwa Mfuko”. Anaeleza Mshomba.

Aidha, Mkurugenzi Mkuu anaishukuru Ofisi ya Waziri Mkuu, Wizara ya Fedha, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumi­shi wa Umma na Utawala Bora, Wadau wa Utatu (ATE, TUCTA, Serikali) Msajili wa Hazina, Mamlaka ya Serikali Mtandao (eGA) na Benki Kuu ya Tanzania kwa usimamizi thabiti wa sekta ya hifadhi ya jamii nchini.

“Nitoe rai kwa waajiri wote nchini kuzingatia sheria za kazi na kutekeleza jukumu la kuwasilisha michango ya watu­mishi wao kwa mujibu wa sheria ili kuwezesha jukumu la ulipaji wa mafao kufanyika kwa hara­ka,” amesema. Mshomba.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *