Mwenyekiti mpya wa Tume ya Umoja Afrika kuchaguliwa Jumamosi hii

Wakuu wa nchi na serikali wa mataifa mbalimbali barani Afrika kuanzia Alhamis ya wiki hii watawasili jijini Addis Ababa nchini Ethiopia, kushiriki kwenye mkutano muhimu wa 38 wa Umoja wa Afrika, kujadili masuala mbalimbali na kumchagua Mwenyekiti mpya wa Tume ya Umoja huo siku ya Jumamosi.

Imechapishwa:

Dakika 2

Matangazo ya kibiashara

Kuanzia uwanja wa ndege wa Addis Abbaba Bole, unaanza kukutana na mabango yanayonadi kikao hicho

Kabla uchaguzi wa uenyekiti wa tume ya AU na naibu wake siku ya Jumamosi,mawaziri na wakuu wa taasisi tofauti chini ya AU watakuwa wanakongamana kutoa ripoti ya mwaka ,maswala ya usalama mdogo na migogoro kwenye ukanda yakitazamiwa kushamiri.

Marais wote pia watakuwa wanahutubia kongamano hilo kabla uchaguzi.

Na katika shughuli ambayo imevutia bara zima ni kinyanganyiro cha uenyekiti kati ya nchi ya Kenya ikiwakilishwa na waziri mkuu wa zamani Raila Odinga, Djibouti ikiwakilishwa na Mahamoud Ali Youssouf huku mgombea wa tatu akiwa ni Richard Randriamandrato kutoka madagascar.

Raila Odinga anayewania uwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika AUC.
Raila Odinga anayewania uwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika AUC. AFP – TONY KARUMBA

Waziri wa mambo ya nje nchini Kenya Musalia Mudavadi ameshawasili Addis huku Raila akitazamiwa alhamisi baada ya kampeni za lala salama katika nchi ya Burundi na Somalia.

Kinyanganyiro kingine pia kinatazamiwa kushuhudiwa katika uchaguzi wa naibu mwenyekiti wa tume hiyo ya AU ambapo mataifa mawili ya Afrika Kaskazini ,Morocco na Algeria  ambayo hayana uhusiano mwema zinakutana kwenye debe.

Mahamoud Ali Youssouf, anayewania nafasi ya uwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika AUC.
Mahamoud Ali Youssouf, anayewania nafasi ya uwenyekiti wa Tume ya Umoja wa Afrika AUC. © diplomatie.gouv.dj

AU ina  nchi wanachama  55    ambazo zinatazamiwa kushiriki kura hizo ,ila kuna mataifa sita ya Burkina Faso, Gabon, Guinea, Mali, Niger  na  Sudan ambazo uanachama wao ulisitishwa kutokana na mizozo ,hivyo hawana ruksha kushiriki.