Mwanga Hakika Bank: Benki inayokua kwa kasi zaidi Tanzania

Dar es Salaam. Kwenye biasha­ra, robo ya nne ya mwaka, ambayo kimsingi ni miezi minne ya mwisho wa mwaka ni wakati wa “kufunga mahesabu ya duka.”

Ni kipindi cha kutathmini mwenendo wa benki kwa mwaka mzima dhidi ya malengo yaliyowe­kwa na uongozi wa taasisi. Mwanga Hakika Bank ni miongoni mwa ben­ki chache zilizofanya vizuri katika robo ya mwisho ya mwaka wa fedha 2023/24.

Katika taarifa yake ya kifedha iliyochapishwa hivi karibuni, ben­ki hiyo imetia fora kwenye vipimo vya kiutendaji wa benki kwa mwa­ka husika kuanzia kwenye faida ya benki, jumla ya mali, amana za wateja, mikopo halisi, mapato ya riba na yasiyo ya riba.

Katika kipindi hicho, faida kabla ya kodi imefikia Sh 15 bilioni kati­ka mwaka 2024 kutoka Sh 10 bili­oni mwaka wa fedha 2023, ikiwa ni ongezeko la asilimia 52.67. Mali za benki zimekua kufikia Sh Sh325 bil­ioni kwa mwaka 2024 kutoka Sh 208 bilioni kwa mwaka 2023, ongezeko la asilimia 56.60.

Jalada la mikopo limefikia tha­mani ya Sh 200 bilioni kwa mwa­ka 2024 kutoka Sh 131 bilioni kwa mwaka wa fedha 2023, sawa na ongezeko la asilimia 52.19 Amana za wateja zimepanda na kufikia Sh 217 bilioni kwa mwaka 2024 kutoka Sh 142 bilioni kwa mwaka 2023, sawa na ongezeko la asimilia 53.24.

Pia, mapato yasiyo ya riba yame­kua kufikia kufikia Sh 10 bilioni kwa mwaka 2024 kutoka Sh 7.2 bilioni kwa mwaka 2023, sawa na ongeze­ko la asilimia 37.3.

Wakati viashiria hivyo muhimu vya benki vikukua, mikopo cheche­fu ya benki imeshuka hadi asilimia 0.87 kwa mwaka 2024 kutoka asili­mia 1.74 kwa mwaka 2023, sawa na anguko la asilimia 50.20.

Akizungumza ofisini kwake, Makumbusho, jijini Dar es Salaam, Mkuu wa Kitengo cha Fedha wa Mwanga Hakika Bank, Chomete Hussein anasema kuwa mwenendo huo wa benki unaashiria kukubal­ika kwao kwa wateja.

“Ukuaji wa amana wa asilimia 53, kutoka Sh 142 bilioni hadi Sh 200 bilioni ni kiashiria cha kwamba wateja wanaamini katika bidhaa na huduma zetu,” anaeleza Hussein.

Ukuaji wa jumla ya mali za benki wa asilimia 56.60, unatuma ujumbe kuwa benki hiyo ndiyo inayokua kwa kasi kwa sasa nchini kwa miaka miwili mfululizo, anasisitiza.

“Utekelezaji mikakati ya benki iliyopo chini ya bodi ya wakurugen­zi sambamba na ubora wa bidhaa umekuwa na nafasi kubwa katika matokeo haya,” anaeleza zaidi Hus­sein.

Pamoja na sababu za ndani za utendaji wa benki, anaamini pia mazingira mazuri ya uwekezaji na ufanyaji biashara yaliyowekwa na Serikali yamechangia wao kufikia hapo.

Kama hiyo haitoshi, anasema usimamizi mzuri katika sekta ya fedha unaofanywa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ni siri nyingine ili­yo nyuma ya hatua hiyo kubwa ili­yopigwa na Mwanga Hakika Bank.

Sehemu maalumu ya wateja na wageni kusubiria huduma katika Benki ya Mwanga Hakika.

Akizungumzia matokeo mazuri ya benki hayo katika mikopo chechefu, anasema kuwa kama benki wamewezesha wafanya­biashara kukopa kiasi cha fedha kinachoweza kuwasaidia kukuza biashara zao ili baadaye warejeshe kwa wakati.

“Ikitokea mkopaji anakopa hala­fu anakutana viashiria vingine vya hatari kama vile mdororo wa kiu­chumi au majanga au anapoach­ishwa kazi, inakuwa ngumu kuli­pa mkopo na kusababisha mkopo chechefu,” anaongeza.

Uimarikaji wa uchumi, usalama wa ajira za wakopaji na uwezo wa watu kutimiza malengo yao, kume­saidia kushuka kwa viwango vya mikopo hiyo chini zaidi ya ukomo uliowekwa kisheria na BoT wa kutokuzidi asilimia tano, hizi ziki­wa sababu za nje.

Ukiingia ndani, anasema ni usi­mamizi mzuri wa mikopo wa benki kuanzia kwenye kutambua biasha­ra za wateja, mahitaji, kiasi cha mkopo na ufuatiliaji wa matumizi ya mkopo na urejeshaji.

“Ukopeshaji kiasi kidogo au uko­peshaji kiasi kikubwa zaidi ni saba­bu ya kuwa na mikopo chechefu; haya ni mambo ambayo kama benki tunayaepuka,” anaeleza Ofisa huyo.

Kutokana na rekodi inazoshi­kilia za kuwa benki inayokua kwa kasi zaidi, anasema hiyo inawapa fursa ya kuendelea kuleta bidhaa bora zinazokidhi mahitaji halisi ya Watanzania.

Fursa zilizotazamwa sokoni

Mwanga Hakika Bank imeona fursa katika maeneo matatu ya kib­iashara; uwekezaji katika teknolojia za kisasa, kundi la wafanyabiashara wadogo na kati na wakandarasi, kulingana na Mkuu wa Kitengo cha Fedha wa benki hiyo.

“Kuna uwekezaji mkubwa wa kidijitali ambao benki inaufanya, ikitoka kwenye majengo kwenda digital, kuhakikisha tunawafikiwa wateja wengi kwa njia ya kidijitali.

“Kundi la SMEs ni kubwa sana hatuwezi kulimaliza lakini ndiyo linaloendesha uchumi wowote ule duniani. Tunatengeneza bidhaa zin­azokidhi mahitaji yao kuhudumia soko hili. Ni soko ambalo limetu­saidia kukua kwa kasi zaidi.

Wakandarasi ni eneo lingine tunaloliangalia kwa makini. Hawa ni wateja wetu kwa muda mrefu na tutaendelea kuwapa kilicho bora,” anadadavua.

Ujumuishi wa kifedha

Anasema mpango wa benki ni kutanua shughuli zake ndani na nje ya mipaka ya nchi licha ya ukweli kwamba upanuzi wake unaangali­wa katika mfumo wa kidijitali, kwa kuangalia mwelekeo wa dunia nzi­ma katika sekta ya fedha.

Anakiri kuwa upanuzi wa matawi hautaachwa na bado ni sehemu ya mkakati wake ambapo baada ya kui­sha kwa robo ya kwanza ya mwaka 2025, wataeleza wapi wanakwenda kufungua matawi. Hivi sasa ben­ki hiyo ina jumla ya matawi saba pekee nchi nzima.

“Mafundi wako chini huko wana­endelea na ujenzi, tukikutana quarter (robo) ya kwanza, mtajua tunakwenda wapi na wapi,” anaele­za zaidi.

Mwelekeo wa benki

Mkakati uliopo ni kufanya maboresho makubwa ya bidhaa za benki ambazo kimsingi huwa hazibadiliki duniani kote. Anase­ma maboresho yatakayofanyika yanahusu Mobile App itakayokuwa na uwezo wa kumpa mteja uzoefu mpya na wa aina yake.

Kingine kinachofanyika, anase­ma, ni kuendelea kubuni na kuonge­za ufanisi wa bidhaa na huduma wanazozitoa kwa wateja.

Changamoto

Hussein anasema kuwa mwaka 2024, soko la huduma za benki lilik­abiliwa na changamoto ya ukwasi, kusababisha kupanda kwa ghara­ma za utunzaji amana za wateja na kuathiri kiwango cha faida ya benki.

Na moja ya ufumbuzi wake, anasema ni kuendelea kuhimi­za watu kuweka fedha zao katika mfumo wa kibenki na kuachana na kuhifadhi majumbani.

“Kukusanya amana kila benki ina­fanya hivyo, lakini unamrahisishia­je mtu kukupa amana. Tulifanya ubunifu mkubwa katika kukusanya amana kupitia mifumo mipya ya malipo. Kwa kufanya hivyo, ukwasi katika benki uliongezeka.”

Shida nyingine ni uhaba wa Dola. Kwa robo tatu yote ya mwaka 2024, Dola ya Marekani iliadimika na kuathiri kiasi kikubwa soko la fedha duniani kote.

Serikali ilipambana kuleta utu­livu wa Shilingi kutokana na kuko­sekana kwa Dola, na wadau kama Mwanga Hakika Bank, walisaidia kuondoa utegemezi wa Dola kwenye uchumi kwa kuleta bidhaa mahsusi kwa wafanyabiashara wanaosafiri­sha bidhaa nje ya nchi kupitia fedha za mikopo ya biashara.

Anasema Watanzania watarajie bidhaa bora za kibenki zinazotat­ua changamoto zao kama ilivyo kawaida yao. Pia, ufanisi na ubunifu utaongezeka maradufu ili kuende­lea kuwahudumia wateja wao.

Kwa wafanyakazi wao, matokeo haya mazuri ni kielelezo cha jasho na nguvu waliyoiweka katika kuhakikisha benki yao inafanya vyema. Mchango wao unathamini­wa.