
KIKOSI cha Mtibwa Sugar kimeendeleza umwamba baada ya kuichapa Cosmopolitan mabao 3-0 wikiendi iliyopita kwenye Uwanja wa Manungu Complex Morogoro, ukiwa ni ushindi wa 14 wa timu hiyo msimu huu katika michezo yake 17, iliyocheza hadi sasa.
Akizungumza na Mwanaspoti baada ya mchezo huo, kocha mkuu wa Mtibwa Sugar, Awadh Juma ‘Maniche’, alisema siri kubwa ya mfululizo wa matokeo chanya ni kutokana na wachezaji wake kujituma na kutambua malengo yao, huku akiwataka pia kutobweteka.
“Ndio mkakati wetu katika kupambania nafasi ya kucheza Ligi Kuu msimu ujao, niwapongeze wachezaji kwa morali na nguvu kubwa wanayoonyesha uwanjani, lazima tuendelee kupambana sana kwa sababu raundi ya pili ndio kwanza imeanza,” alisema.
Kocha huyo anayeiongoza timu hiyo baada ya kuondoka Mmarekani Melis Medo aliyetua Kagera Sugar, tangu ilipotoka sare ya kufungana mabao 2-2, ikiwa ugenini dhidi ya Biashara United, Novemba 16, mwaka jana, imeshinda michezo minane mfululizo.
Timu hiyo kwa sasa inaongoza katika Ligi ya Championship ikiwa na pointi zake 44, baada ya kucheza michezo 17, ikishinda 14, sare miwili na kupoteza mmoja tu, ambapo imefunga jumla ya mabao 31, huku ikiruhusu nyavu zake kutikiswa mara saba.