
Dar es Salaam. Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (Zipa) imesema Kongamano la uwekezaji litakalofanyika Mei 7,2025 visiwani humo, litakuwa lango la wawekezaji wa ndani na nje ya nchi kutafuta fursa ambazo hazijatumika visiwani humo.
Kongamano hilo lina kaulimbiu isemayo, “Ni wakati wa Pemba” dhamira kuu ni kuweka mikakati ya kukuza kiuchumi kisiwamo humo.
Hayo yameelezwa leo Aprili 17, 2025 na Mkurugenzi Mtendaji wa Zipa, Saleh Saad Mohamed wakati akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Mohamed amesema kongamano hilo litakalofanyika Mei 7 hadi 10, 2025 ni sehemu ya utekelezaji wa dira ya kiuchumi ya Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Mwinyi, inayolenga kukuza uchumi wa Zanzibar na kuufanya kuwa kitovu cha maendeleo endelevu kanda ya Afrika Mashariki na kwingineko.
“Mkutano huu siyo tukio la kawaida. Ni fursa ya kipekee kwa wawekezaji wa ndani na nje kutambua fursa mpya na kufanya ushirikiano wa kimkakati katika sekta za kipaumbele zinazojenga mustakabali wa Pemba,” amesema.
Mohamed amesema kongamano hilo litakuwa na washiriki 750 wakiwemo wakurugenzi wakuu wa kampuni za kimataifa, wawekezaji, wanadiplomasia na viongozi wa Serikali
Amesema mkutano huo utajumuisha maonyesho ya biashara ya siku mbili, mijadala ya kitaalamu kuhusu fursa za uwekezaji.
Mkurugenzi huyo ametoa wito kwa sekta binafsi na taasisi za umma kuchangamkia fursa ya uwepo wa kongamano hilo kuonyesha ubunifu wao, kuungana na wawekezaji na kujenga ushirikiano wa kimkakati utakaosaidia kufikia malengo ya maendeleo.
“Tunajenga uchumi shirikishi, na mkutano huu ni kielelezo cha dhamira yetu ya kujenga mazingira ya uwekezaji ya kiwango cha kimataifa kupitia uwazi, mijadala yenye manufaa. Tunakaribisha kila mtu kuungana nasi na kuwa sehemu ya hadithi ya mabadiliko ya kiuchumi ya Pemba,”amesema.