Jamhuri Park mpya yaleta tabasamu kwa vijana na jamii jijini Tanga

Kwa miaka mingi, Jam­huri Park maarufu kama Forodhani ilikuwa sehemu isiyopewa kipaumbele jijini Tanga, ikiachwa na nyasi kavu, taka, na ukosefu wa usimamizi madhubuti. Lakini leo hii, bustani hiyo ya ekari 7.7 iliyoko barabara ya Uhuru mjini Tanga, ni mfano hai wa mabadiliko yanayowezekana kupitia ushirikiano wa jamii na uon­gozi wenye maono.

“Kuhusu Jamhuri Park, tulikuwa tunaona ni seh­emu ya kupita tu, hakukuwa na chochote cha kutuvu­tia,” anasema Zuhura Has­san, mkazi wa Mwanzange. “Sasa, kila Jumamosi tunakuja hapa kupumzika na watoto.” Ushuhuda wa Zuhura unaakisi maelfu ya wakazi wa Tanga walio­pokea kwa mikono miwili ukarabati wa bustani hiyo chini ya programu ya Tan­gaYetu.

Kabla ya mwaka 2023, Jamhuri Park haikuwa kivu­tio tena. Iliathirika na ucha­kavu, kutotunzwa, na ukose­fu wa huduma muhimu kama taa, vyoo vya kisasa, na maeneo ya michezo kwa watoto. Bustani hiyo hai­kuchangia chochote kwenye pato la Halmashauri ya Jiji la Tanga.

Muonekano wa kauvutia katika eneo la Jamhuri Park maarufu kama Forodhani.

Kupitia programu ya Tan­gaYetu, kwa ushirikiano na Halmashauri ya Jiji la Tan­ga, bustani hiyo ilifanyiwa mchakato jumuishi uliohu­sisha wananchi, vijana, na wadau wengine kupanga kwa pamoja muundo mpya wa bustani hiyo. Mradi huo ulijumuisha upembuzi yaki­nifu, uandaaji wa mpango wa biashara, na ukarabati mkubwa wa miundombinu.

“Lengo letu halikuwa tu kuboresha miundombinu ya mijini,” anasema Prof. Ally Namangaya, aliyesi­mamia awamu ya usanifu wa bustani hiyo. “Tulitaka kuleta mabadiliko ya kweli kuhusu jinsi miji yetu ina­vyowahudumia wakazi wake, hasa vijana. Leo hii, Jamhuri Park si bustani tu, bali pia ni kitovu cha biasha­ra, burudani kwa watoto na vijana, na umoja wa jamii”.

Bustani kwa sasa ina seh­emu za kijani za kupumzi­ka, maeneo ya michezo ya watoto yenye vifaa vya kisasa, vibanda vya biasha­ra kwa wajasiriamali vijana, taa zinazotumia nishati ya jua, na mfumo wa usi­mamizi wa taka. Watoto hushiriki michezo, watu wazima hukutana kwa mazun­gumzo na kupunga upepo wa Bahari ya Hindi, na wafanyabiashara huuza bidhaa mbalimbali.

Kwa mujibu wa Bwa­na Jonas Ngwatu, Afisa Biashara wa Jiji la Tanga na msimamizi wa bustani hiyo, zaidi ya vijana 50 wamepata nafasi za kuendesha biashara zao nda­ni ya bustani hiyo. “Jam­huri Park ni seh­emu ya kukaribisha watu wa rika zote. Watoto wana­furahia michezo, wazazi wanapumzika, na vijana wanauza bidhaa zao kwe­nye vibanda rasmi,” anas­ema.

Wakati wa ujenzi, zaidi ya vijana 30 walihusishwa kwenye kazi za muda mfu­pi katika ujenzi, usafi hadi kazi za kiufundi. Bustani hiyo pia imekuwa sehemu kuu ya matukio ya kijamii, mikutano na tamasha, jam­bo lililoongeza mapato ya Halmashauri ya Jiji la Tanga kwa kiasi kikubwa.

Meya wa Tanga, Mhe. Abdurahman Shiloow, anas­ema, “Jamhuri Park inaakisi dhamira ya Tanga ya kuleta maendeleo na mshikamano. Hili ni darasa kwa miji min­gine nchini.”

Jamhuri Park imekuwa somo la jinsi maeneo ya umma yakitumiwa vizuri yanaweza kuimarisha mshikamano wa jamii, kukuza uchumi wa ndani, na kuwapa vijana nafasi ya kujitegemea. Mradi huu umekuwa mfano kwa miji kama Dodoma, Tunduma, na Mwanza ambapo mae­neo ya wafanyabiashara wadogo yameanzishwa kwa kuiga mfumo huu wa ush­irikishwaji.

Kwa Tanga, bustani hii sasa ni ahadi iliyotim­izwa. Inawakumbusha wananchi kwamba mab­adiliko yanawezekana pale ambapo jamii na viongozi wanashirikiana.

Programu ya TangaYetu inafadhiliwa na Fondation Botnar na inatekelezwa na kampuni ya INNOVEX (www.innovexdc.com) kwa kushirikiana na Hal­mashauri ya Jiji la Tanga, ikiifanya Tanga kuwa jiji ambalo vijana wanastawi.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *