#HABARI: Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Innocent Bashungwa, ametoa wito kwa Waandishi wa habari kuendelea kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha na kuwakumbusha Watanzania juu ya umuhimu wa tunu ya amani na usalama, ambayo ni urithi kutoka kwa waasisi wa taifa letu, Tanzania.
Ametoa wito huo wakati akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kufungua Mkutano wa Wakuu wa Majeshi ya Polisi kutoka Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), unaofanyika katika ukumbi wa JNICC – Dar es Salaam, leo tarehe 5 Juni, 2025.
“Niendelee kuwaomba, muendelee kushirikiana na Serikali kwa kuwakumbusha Watanzania kuwa amani ni tunu ambayo waasisi wa taifa letu wametuachia, na ulinzi wa taifa letu ni jukumu la kila Mtanzania,” amesema Bashungwa.
Bashungwa amesisitiza nafasi ya vyombo vya habari katika kufanya uandishi wa uchunguzi (investigative journalism), ili kuwaonesha Watanzania hali halisi ya mataifa yanavyopata shida kutokana na kukumbwa na migogoro iliyopelekea amani kutoweka.
Aidha, Bashungwa ametoa wito kwa Watanzania kuendelea kulinda nchi kwa uzalendo mkubwa, mshikamano na utulivu, na kuifanya Tanzania kuendelea kuwa kisiwa cha amani.
Ametumia nafasi hiyo kumshukuru Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuviwezesha vyombo vya usalama, ikiwa ni pamoja na Jeshi la Polisi, kwa kuhakikisha usalama wa raia na mali zao unaendelea kuimarishwa.
Kadhalika, Bashungwa amesema Tanzania inaendelea kuimarisha ushirikiano na nchi za SADC katika kupambana na uhalifu.
Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Polisi Nchini (IGP), Camillus Wambura, amesema mkutano huo wa Wakuu wa Majeshi ya Polisi wa nchi za SADC utajadili na kujipanga kwa pamoja kupambana na uhalifu mkubwa wa kupanga na unaovuka mipaka, ili kwa pamoja kuzuia matukio ya kihalifu katika nchi hizo.
#itvdigital #itvupdates #itvtanzania.
#follow @radioonetanzania