
Mashambulizi ya Israel na Iran yameongeza bei ya mafuta duniani kufikia $100 kwa pipa.
Hofu kubwa duniani ni katika usafirishaji wa mafuta na gesi kupitia njia ya bahari ya Hormuz.
Hii ni kwa sababu, iwapo mapigano yataendelea Iran inaweza kuamua kufunga njia muhimu ya bahari inayoitwa Hormuz, ambayo ndiyo inayotumika kupitisha bidhaa mbalimbali, ikiwemo mafuta ghafi, gesi na hata makontena.
16 Juni 2025 Oparesheni za Biashara ya Bahari ya Uingereza (UKMTO) ilisema Jumatatu ilipokea ripoti nyingi za kuongezeka kwa mwingiliano wa kielektroniki katika maji ya Ghuba na Mlango wa Hormuz.
Iliongeza kuwa uingiliaji huo unaathiri kwa kiasi kikubwa utoaji wa taarifa za meli kupitia mifumo ya kiotomatiki.
Ikiwa Tehran itaamua kuzidisha mzozo huo kwa kulipiza kisasi nje ya mipaka ya Israeli, inaweza kujaribu kuufunga Mlango-Bahari ya Hormuz, lango muhimu zaidi ulimwenguni la usafirishaji wa mafuta.
“Tuna ripoti kwamba wamiliki zaidi wa meli sasa wanatumia tahadhari zaidi na wanaamua kukaa mbali na Bahari Nyekundu na Ghuba ya Persia,” alisema Jakob Larsen, afisa mkuu wa usalama na usalama wa chama cha meli cha BIMCO.
Iran, ambayo imekanusha nia kama hiyo, siku za nyuma ilitishia kufunga Mlango-Bahari wa Hormuz kwa kulipiza kisasi shinikizo la Magharibi.
Wataalam wamesema kuwa kufungwa kwa njia yoyote ya bahari kunaweza kuzuia biashara na kuathiri bei ya mafuta duniani.
Usafirishaji wa Hormuz
Bidhaa zinazosafirishwa kupitia mlango wa bahari wa Hormuz zinakwenda katika maeneo mbalimbali ya dunia, ikiwemo barani Afrika. Hormuz ni njia nyembamba ya bahari na ndiyo njia pekee inayoingia katika Ghuba ya Persia.
Inaigawa Iran upande mmoja na Oman na Falme za Kiarabu kwa upande mwingine. Njia hii pia inaunganisha Ghuba ya Persia na Ghuba ya Oman na Bahari ya Arabia hadi Bahari ya Hindi.
Iko katikati ya Oman na Iran na inatumika kama mfereji muhimu wa kuunganisha wauzaji mafuta ghafi katika Ghuba ya Mashariki ya Kati na masoko ya kimataifa.
Takriban mapipa milioni 20 ya mafuta hupita kila siku, kupitia mlango wa Hormuz, hii ni zaidi ya 35% ya biashara ya mafuta ghafi duniani.
Upana wake ni kati ya kilomita 55 na 95 Mafuta haya yanasafirishwa hadi Bahari ya Hindi kwa usafiri zaidi wa baharini.
Iwapo Hormus itafungwa, basi wafanyabiashara wanaweza kuamua kutumia njia mbadala, lakini itakuwa ni kwa gharama kubwa zaidi, hivyo kuwa na athari ya moja kwa moja kwa watumiaji.
“Hormuz ni njia muhimu ya maji, isiyo na mbadala, kwa biashara ya meli za mafuta na kizuizi chochote au tishio kwa usafirishaji huru wa meli itakuwa na athari kubwa kwa uchumi wa dunia,” chama cha usafirishaji wa meli za mafuta INTERTANKO kilisema.
Wazalishaji wote wakuu wa mafuta wa Mashariki ya Kati ikiwemo Saudi Arabia, Iran, Umoja wa Falme za Kiarabu, Kuwait, na Iraq wanategemea sana njia hii. Mlango huo wa bahari uliwahi kufungwa kwa muda Fulani wakati wa vita vya Iran na Iraq kati ya 1980 na 1988.
Kiasi kikubwa cha shehena kutoka bandari hizi zinapelekwa Dubai, ambayo imekuwa kitovu cha usafirishaji wa mizigo na njia ya mizigo kufikia Ghuba ya Persia, Asia Kusini, na Afrika Mashariki.
Mvutano wa sasa kati ya Iran na Israel pia inawalazimisha wamiliki wa meli na waendeshaji kuangalia uhusiano wa meli zao na Israeli kabla ya safari zao za Bahari ya Arabia, Ghuba ya Oman, na Ghuba ya Arabia.
Hata meli zilizokuwa na uhusiano wa zamani na Israel huenda zikashambuliwa.Hivyo, wakati mashambulizi kati ya Israel na Iran yakipamba moto.
Dunia inaiangalia Hormuz na kutafakari athari ya njia hiyo kufungwa.Kwa sababu, kutatizika kwa usafirishaji wa mafuta ghafi kutakuwa na athari kubwa katika soko la kimataifa ikichochea mfumko wa bei za bidhaa na kuyumba kwa uchumi.
Mpaka sasa, haijafahamika iwapo Iran itaamua kuifunga njia hiyo au la, ni suala la kusubiri na kuona.