Harmonize anavyotumia kivuli cha Diamond kupiga hela

Dar es Salaam. Licha ya ugomvi wao miaka ya hivi karibuni, hilo haliondoi ukweli kuwa Staa wa Konde Music Worlwide, Harmonize anamtazama Diamond Platnumz kama mfano wa kuigwa (role model) katika muziki, biashara na mtindo wa maisha.

Utakumbuka Diamond ndiye alimtoa Harmonize kimuziki mwaka 2015 kupitia WCB Wasafi akiwa ni msanii wa kwanza kumsaini katika rekodi lebo yake hiyo ambayo kwa sasa inasimamia wasanii wanne.

Mchakato wa Harmonize kuachana na WCB Wasafi mwaka 2019 ulizaa uhasama kati yao, vita vya maneno vikachukua nafasi hasa mtandaoni huku kila upande ukitupa shutuma kwa mwenzake.

Hata hivyo, bado Diamond ni kioo anachojitazama Harmonize na kuona wapi anaweza kurekebisha na wapi ataboresha, hatua hiyo imepekekea Harmonize kufanana mambo mengi na Diamond katika muziki, biashara na mtindo wa maisha kama ifuatavyo,

Mosi; baada ya Diamond kupata umaarufu kimuziki alianzisha uhusiano na Wema Sepetu, Miss Tanzania 2006 na Staa wa filamu ambaye alimtumia katika video ya wimbo wake, Moyo Wangu (2011).  

Kwa upande wake Harmonize baada ya kuwa maarufu alizama katika penzi na Staa wa filamu Bongo, Jacqueline Wolper ambaye alimtumia katika video ya wimbo wake, Niambie (2017).

Pili; Diamond alianzisha WCB Wasafi baada ya kuondoka Sharobaro Records, hiyo ni sawa na Harmonize aliyeanzisha Konde Music baada ya kuondoka WCB Wasafi, na wote kuhama kwao kulizusha kutoelewana na Mabosi wao wa mwanzo.

Hata hivyo, wawili hao walikuja kukutana na kitu kama hicho, wasanii walitoka katika lebo zao na kwenda kuanzisha na zao, Rich Mavoko aliondoka WCB Wasafi na kuanzisha Billionea Kid, huku Country Boy akiondoka Konde Musc na kuanzisha I AM Music.

Tatu; katika kunogesha biashara yake ya muziki, Diamond aliamua kujipa jina la ‘Dangote’ ambaye ni tajiri mkubwa wa Nigeria na Afrika nzima, Harmonize naye akapita humo humo kwa kujipa jina la ‘Bakhresa’ ambaye ni tajiri mkubwa Tanzania na Afrika.

Ukiwasikiliza wasanii hao wakiyataja majina hayo kwenye nyimbo zao utadhani ni ya kwao kweli, kumbe wapi! ni kutaka kuonyesha ni jinsi gani ni wakubwa kimuziki kama matajiri hao upande wa biashara.

Nne; baada ya kuondoka WCB Wasafi, Harmonize alifichua kuwa lebo hiyo ilimpa mkataba wa miaka 10 na katika mapato lebo ilikuwa inachukua asilimia 60 na yeye kama msanii asilimia 40.

Hata hivyo, Anjella ambaye ameondoka Konde Music amesema mkataba wake ulikuwa wa miaka 10 na mgawanyo wa mapato ulikuwa ni asilimia 60 kwa 40, kama ni hivyo, basi Harmonzie ‘kakopi na kupesti’ kutoka kwa Diamond!.

Tano; ili kuonyesha yeye ni mkali wa katika muziki, Diamond alijipachika jina la ‘Simba’ moja ya wanyama wakali na tishio mwituni, Harmonize naye hakucheza mbali, akajipachika jina la ‘Tembo’ ambaye hana wa kumtisha mwituni.

Utakumbuka hilo ndilo lilipelekea na Rayvanny kujipachika jina la ‘Chui’ ambaye anaogopeka mwituni, wasanii hao wanatumia majina hayo kama chapa zao na mara nyingi wamekuwa wakiyataja katika nyimbo zao.

Sita; hadi sasa Diamond kafanya video na warembo watatu ambao aliwahi kuwa nao katika mahusiano, Wema Sepetu – Moyo Wangu (2011), Hamisa Mobetto – Salome (2016) na Zari The Bosslady aliyefanya naye video mbili, Utanipenda (2015) na Iyena (2018).

Harmonize naye akapita njia hiyo hiyo, ameshafanya video na warembo wake watatu aliowahi kuwa nao, Jacqueline Wolper – Niambie (2017), Kajala Masanja – Nitaubeba (2022) na Sarah aliyefanya naye video mbili, My Boo Remix (2019) na Niteke (2019).

Saba; baada ya kufanikiwa kimuziki, Diamond aliingiza sokoni bidhaa zake kupitia chapa yake, alikuja na Chibu Perfume, Wasafi.com na Diamond Karanga, ni miradi iliyopata mapokezi mazuri kipindi cha mwanzo ila baadaye ikapotea.  

Naye Harmonize baada ya kundoka WCB Wasafi alitaka kufanya mambo kama hayo, alitangaza ujio wa bidhaa zake za sigara, ‘Tembo Cigarate’ na kuomba wafanyabiashara kujitokeza ili kushirikiana katika mradi huo ambao hadi leo bado haujaanza.

Ikumbukwe hadi sasa Diamond hajawahi kumshirikisha Harmonize katika wimbo wake wowote ule ila Harmonize amefanya hivyo katika nyimbo zake tatu, Bado (2016), Kwangwaru (2018) na Kainama (2019) ambao pia Burna Boy alishirikishwa.
 

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *