Fyatu afyatua figa na fwakit kuhusu Kanada

Tangu nifyatukie Kanada, nimekuwa nashuhudia mambo ya ajabu toka kwa mafyatu. Wapo wanaoomba mialiko ili waje huku wagome kurejea kwao na kufanya niwatunze hadi nifyatuke.

Wapo wanaonipiga mizinga tena mingine ya kijinga siyo kifyatu. Hivi, unajisikiaje fyatu ambaye ameishastaafu kukubomu dolari 500 kwa ajili ya harusi ya kitegemezi chake na si kwa ajili ya matibabu yake?

Akili au matope?

Kwa nini kuoa, kuoza na kuozwa kwa mifuko ya mafyatu? Je, wao walipooa au kuolewa uliwachangia lau moja ya kumi ya hizo unazoitisha?

Ajabu ya maajabu, siku hizi, mafyatu wanaweka hata kiwango cha chini cha nchango wa harusi kana kwamba wanajua una kiasi gani benki au uchagoni!

Hakuna mafyatu waliokosa ubunifu kama wangu. Hata mamlaka zinahangaika na njuluku za madiaspora wakati haziwatendei yoyote zaida ya ntima nyongo.

Ukitaka kujua huu ni ukumbaff, sorry, unyonyaji na uzwazwa, itisha nchango wa kupeleka kitegemezi shule au mgonjwa hospitalini, hawajachangii. You know what? Loo! Nimesahau naongea na mafyatu wa kibongo na si wa kitasha siyo!

Hayo ya kimombo na watasha tuyaache. Ukichunguza nchango, wengi hawachangii harusi wala nini bali kupata fursa ya kula, kunywa, na kufanya mambo yao.

Kwa mafyatu wanaopenda kudumisha mila, wanajua ninachomaanisha hapa au siyo? Wanajificha migombani na kumaliza mambo yao.

Kwa ufupi, ni kwamba hawakuchangii harusi wala wewe bali wanajichangia kwa kisingizio cha kukuchangia. Ni ajabu.

Wavyele wengi hawaipati hii. Chao ni kujisifu kuwa harusi ilinoga wakati yote ni malengo na mifuko ya mafyatu wasioona mbali.

Kwa nini hiyo njuluku mnayounguza kwenye utopolo kama harusi msiichangie kwenye kununua hisa hata kwenye masoko ya njuluku?

Turejee kwa Kanada au Kanuki kama waiitavyo wenye kaya yao, hasa wale originali siyo sisi wa nkorogo tuishio kwa vibali vya ukazi hata watasha walioivamia na kuitwaa na kuigeuza yao kiasi cha kutuuliza sisi nyie mwatokea wapi kana kwamba wao si wakuja kama sisi.

Kanada ina ukubwa wa kilomita za mraba 9,093,507 ikilinganishwa na Bongo yenye 947, 303.

Hii maana yake ni nini? Ni kwamba Kanada inaimeza mara tisa na nusu na ushei.

Mkoa (Himaya) mkubwa kuliko yote Kanada wa Nunavut unaweza kuimeza Bongo mara mbili na ushei kwa ukubwa wa kilomita za mraba 2,093,190. Jiulize.

Pamoja na ukubwa wote huu, ina mafyatu wangapi? Cheka taratibu. Ina jumla ya mafyatu 41, 414. Kama mafyatu wa Nanavut wakiamua kugawana himaya wao, kila mmoja atapata si chini ya kilometa 30 za mraba kama shamba lake ikilinganishwa na Bongo ambapo kila mbongo atapata kilometa za mraba 14. Kwa Visiwani, kila mmoja atapata 000.13!

Shangaa sasa. Hata mkoa mdogo kuliko yote wa Kanada wa Prince Edward Island (PEI) wenye ukubwa wa kilomita za mraba 5,660 ni mkubwa kuliko Visiwani yenye ukubwa wa kilomita za mraba 2, 462 ambayo ni mara mbili na ushei.

Je, wajua kuwa Visiwani ni 1 ya 383 na ushei ya Bara? Ajabu, zote mbili zina haki sawa katika muunganiko! Ukiuliza mantiki, sijui kama utapata jibu lifyatualo akili zaidi ya siasa na sanaa.

Katika siasa, moja na 400 ni sawa! Japo sina takwimu, ukweli ni kwamba wazenj wengi, kupitia mgongo wa muungano wa mnyonyano, sorry mpendano, wapo wengi bara kuliko visiwani.

Ni udugu na upendo kiasi gani kiasi cha 1/383 kutoa hata mnene wa kaya? Du! Ningekuwa braza Mtikisa wa Tikisa gabacholi, ningeuliza. Je, nani iko roga nyinyi ambaye nanyonwa lakini haipo fanya hesabu na hoji dugu yangu?

Ukija kwenye pato la jumla la Kanada, ni Dola 37, 317 ikilinganishwa na Bongo yenye dolari 2,500.

Hii maana yake ni nini kifyatu? Ina maana Mkanada mmoja ana uwezo wa kiuchumi mara 15 ya fyatu wa Kibongo.

Ajabu, mafyatu wa Kikanada hawachangishani kwa ajili ya harusi. Je, wajua Kanada ina idadi ya mafyatu wangapi? Jibu ni rahisi.

Ina 41,528,680.

Siombi msamaha kwa wale wanaochukia namba. Wapo waliodhani kuwa Fyatu Mfyatuzi hajui kuzifyatua namba kwa vile ni mwanasharia na mwandishi wa umbea.

Kwenye namba, nilikuwa nampa taabu ticha wangu zama zile za ujima. Wengi hawajui kuwa nina tuzo ya Nobo ya namba!

Pia, nina tuzo ya juu ya takwimu. Nina uwezo wa kufanya mahesabu hata ya maji na uji na namna unavyoingia tumboni mwa mafyatu.

Nina uwezo wa kuhesabu matone ya mvua na michanga ya bahari.

Unadhani natania? Niulize michanga ya bahari au matone ya mvua ni kiasi gani. Hata usipouliza, acha nikupe jibu la kimahesabu kuwa ni mengi na mingi. Kkkk. Umenipata siyo?

Una habari kuwa mimi ndiye niligundua formula ya mahesabu kuhusiana na idadi ya vitu. Mimi ni mgunduzi na mvumbuzi wa fomula ya ingi. Hivi, nimesemaje?

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *