
Klabu ya soka ya Simba ya Tanzania inajitupa uwanjani leo Jumamosi kuikaba koo Klabu ya RS Berkane ya nchini Morocco katika mchezo wa duru ya kwanza ya fainali ya kuwania kombe la shirikisho barani Afrika.
Simba inatafuta ushindi wa kufa na kupona ili kuandika historia ya kuwa klabu ya kwanza ya Tanzania kubeba kikombe cha moja ya mashindano makubwa ya kandanda barani Afrika. Klabu hiyo ilicheza fainali yake ya mwisho ya mashindano ya ngazi ya bara zima mwaka 1993.
Kocha wa Simba, Fadlu Davids amesema wanatambua umahiri wa Klabu ya RS Berkane lakini wamedhamiria kuuonesha ubavu watakapoteremka dimbani baadaye hii leo.
Kocha ya Berkane Mouin Chaabani amejitapa kwamba haoni sababu ya klabu yake kutonyakua kikombe hicho. Mchezo wa duru ya pili utapigwa Mei 25 nchini Tanzania.