Kakola. Kamati Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) inatarajiwa kukutana jijini Dar es Salaam Jumatano Mei 21, 2025.
Kikao hicho kimeitishwa kipindi ambacho chama hicho kinapitia misukosuko ikiwemo ya mwenyekiti wake, Tundu Lissu kuwa gerezani akikabiliwa na kesi mbili ya uhaini na ya kuchapisha taarifa za uongo mitandaoni.
Pia, makada na viongozi wake kuanzia ngazi ya kamati kuu, kanda, mikoa, wilaya, majimbo hadi kata wakitangaza kukihama kwa madai kimepoteza mwelekeo.
Aidha, kamati kuu hiyo imeitishwa kipindi ambacho Ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa imeiandikia barua Chadema ya kuwaeleza kutokuwatambua viongozi wanane wa kamati kuu na sekretarieti.

Hiyo inatokana na kudai akidi ya Baraza Kuu la Januari 22, 2025 haikutimia na kuwataka kuitisha upya baraza hilo. Miongoni mwa viongozi hao ni Katibu Mkuu, John Mnyika na naibu wake wawili Bara na Zanzibar.
Tangu kumalizika kwa mkutano mkuu wa uchaguzi wa chama hicho, Januari 22, 2025 na Lissu kuibuka mshindi wa uenyekiti dhidi ya Freeman Mbowe aliyekuwa anatetea nafasi hiyo aliyoishika kwa miaka 21, chama hicho kimekuwa na mivutano ya ndani kwa ndani.
Aidha, kikao hicho kimeitishwa Makamu Mwenyekiti wake Bara, John Heche kipindi ambacho makada na viongozi wake wanaokikimbia wakieleza Heche ameshindwa kukiongoza vyema kwa vikao badala yake kimekuwa cha matamko.

Makamu Mwenyekiti wa Chadema, John Heche akihutubia mkutano wa hadhara Kijiji cha Mwakitolyo Wilaya ya Shinyanga. Picha na Peter Saramba.
Alhamisi ya Mei 15, 2025, Mwenyekiti wa Kanda ya Kati, Devotha Minja wakati akitangaza kujiuzulu alisema tangu Lissu akamatwe, wanachama wao waumizwe mahakamani Heche ambaye ndiye kiongozi mkuu wa chama hicho ameshindwa kuitisha kamati kuu.
Devotha ambaye naye alikuwa mjumbe wa kamati kuu alisema kamati kuu inaweza kujadili na kutoka na mwelekeo wa namna ya kwenda lakini hilo limeshindikana.
Siku moja kupita yaani jana Ijumaa, Mei 16, 2025, Heche akizungumza na wanachama wa Chadema Famili Kijiji cha Kakola wilayani Kahama mkoani Shinyanga katika kikao cha ndani alitangaza uwepo wa kikao hicho.

Amesema kikao hicho kitajadili mambo kadhaa ya ustawi na mikakati ya chama ikiwemo muendelezo wa kampeni ya No reforms, no election ‘bila mabadiliko hakuna uchaguzi’ ambayo imefanyika kanda mbalimbali za chama hicho.
“Kuna watu eti wanadai Chadema inakufa…Chadema hii hii tunayoitisha mkutano wa hadhara saa 2:00 asubuhi na watu wanajitokeza hadi mtu unakosa pa kukanya ndio inakufa? Wanajidanganya sana,” amesema Heche
Bila kutaja ajenda za kikao hicho, Heche amesema: Mei 19, 2025 tunaenda Mahakama ya Kisutu kwenye kesi ya Mwenyekiti wetu Tundu Lissu na Mei 21 tutafanya kikao cha Kamati Kuu. Baada ya hapo tutaueleza umma nini kinafuata. Chadema siyo tu ni chama cha siasa, Chadema ni imani katika mioyo ya Watanzania wapenda haki na demokrasia.”
Amesema kikao hicho kitafuatiwa na kikao cha Baraza Kuu ambacho hata hivyo hakutaja kitafanyika lini.
“Wamemkamata na kumweka ndani Lissu kwa kesi ya uhaini wakidhani tutatetereka kwa kujifungia ndani kulia, sasa wanashangaa kuona kampeni ya No reforms, No election inachanja mbuga,” amesema.
Heche amesema wana timu mbili ambazo ni ile anayoingoza yeye (Heche) na Katibu Mkuu, John Mnyika:”Zshambulia kila kona kudai mabadiliko.”
Amewahakikishia makada wa chama hicho hakuna nguvu ya dola, vitisho, kesi wala kuta za magereza zitakazowarejesha nyuma ari na nia ya Chadema kudai mabadiliko ya kisheria yatakayoweka sawa uwanja wa siasa kwa wagombea na vyama vyote.
“Naapia mimi na viongozi wenzetu hatutarudi nyuma katika mapambano ya kudai haki na maisha bora kwa Watanzania,” amesema Heche.