
Nchini Burkina Faso, wiki iliyopita ilishuhudia kukamatwa kwa maafisa kadhaa wa jeshi, wawili kati yao walifutwa kazi kama makamanda. Ingawa hakuna mawasiliano bado yamefanywa kuhusu suala hili, wafuasi kadhaa wa utawala wa kijeshi wanazungumza kuhusu jaribio la mapinduzi ya kijeshi, wakiwanyooshea kidole askari walio uhamishoni.
Imechapishwa:
Dakika 1
Matangazo ya kibiashara
Nchini Burkina Faso, miongoni mwa maafisa waliokamatwa ni Hakimu Kamanda Frédéric Ouédraogo, kamanda wa zamani wa Kikosi cha mahakama ya Kijeshi. Kulingana na vyanzo vya usalama, kamanda huyo alikuwa akichunguza mauaji ya kamanda Ismaël Touhogobou, ambaye alishukiwa kuhusishwa na jaribio la mapinduzi, aliyepigwa risasi na kufa papo hapo mwezi Oktoba 2023. Wakati huo, mwendesha mashtaka wa kijeshi alidai kuwa operesheni ya “kuwakamata washukiwa ilikwenda vibaya.”
Kwa upande wake, Kapteni Elysée Tassembedo, aliyepewa jina la utani “mkombozi wa Sebba”, kamanda wa Kundi la Kikosi cha Usalama cha eneo la Kaskazini kilichopo Ouahigouya, alikamatwa alipokuwa Ouagadougou, kwa mkutano ulioitishwa na makao makuu ya jeshi, maudhui ya majadiliano ambayo bado hayajajulikana.
Maafisa kadhaa wa kijeshi walibadilishia nafasi zao
Hali hiyo ilimfanya Rais wa Mpito, Kapteni Ibrahim Traoré, kuchukuwa hatua ya haraka kuwabadilishia nafasi za kazi maafisa kadhaa. Ingawa idadi yao kamili haijajulikana, wanajeshi wengine waliripotiwa kukamatwa. Wafuasi wa utawala wa kijeshi tuliowasiliana nao wanazungumzia jaribio jingine la mapinduzi. Baadhi ya maafisa serikalini wananyooshea kidole cha lawama maafisa wa zamani ambao pia walitimuliwa katika jeshi. Kwa sababu hii, vyanzo vya usalama vinasema kuwa hali ndani ya jeshi la Burkina Faso bado ni ya wasiwasi.