
Rais Ruto amesema tukio hilo kufanyika mikononi mwa polisi ni jambo linalosikitisha na lisilokubalika huku akitoa wito kwa polisi kushirikiana kufanya uchunguzi huru dhidi ya mauaji ya kijana Albert Ojwang.
Polisi awali ilisema mwanablogu huyo Albert Ojwang, aliyekamatwa kutokana na maandiko yake katika mitandao ya kijamii, yaliyomshutumu naibu inspekta mkuu wa polisi kwa rushwa, alifariki dunia baada ya kugonga kichwa chake ukutano akiwa kizuizini. Hata hivyo Bernard Midia daktari wa upasuaji wa maiti alikanusha ripoti za Albert Kujiua.
Mpasuaji: Mwanablogu Kenya alifariki kwa kupigwa kichwani
“Lakini damu tulizozikuta kichwani na kwenye ngozi ya kichwa chake, zilikuwa zimetapakaa sehemu zote, ikiwemo uso, pembeni mwa kichwa chake na hata nyuma ya kichwa. Tukiangalia na majeraha mengine aliyoyapata mwilini mwake hakika hawezi kuwa amejidhuru mwenyewe,” alisema Midia.
Rais Ruto hata hivyo amesema anatarajia ukweli kujua kile kilichojiri wakati wa kifo chake na haki kutendeka. Mauaji ya Ojwang yanakuja wakati Kenya ikiwa katika tahadhari kubwa wakati ikiadhimisha mwaka mmoja tangu kutokea maandamano makubwa ya Gen Z, kupinga rushwa na ongezeko la kodi.