
Jeshi la Sudan Kusini limesema litaanzisha zoezi la kukusanya silaha kutoka kwa vijana watakaokuwa tayari kusalimisha kwa khiyari katika maeneo ambayo yako chini ya sheria ya hali ya dharura.
Jeshi hilo limesema baada ya zoezi hilo, utafuata mchakato wa kuwapokonya watu silaha kwa lazima utakaofanywa na kikosi maalum katika kaunti za Warrap na Mayom, ambako wiki iliyopita Rais Salva Kiir alitangaza hali ya dharura kufuatia khofu ya usalama kwa kipindi cha miezi sita.
Maeneo hayo yanakabiliwa na ongezeko kubwa la machafuko ya kikabila yakihusisha wizi wa mifugo. Msemaji wa Jeshi la Ulinzi la Sudan Kusini, Lul Ruai Koang, amewaambia waandishi habari tayari kikosi cha kusimamia zoezi la ukusanyaji silaha kimepelekwa kwenye maeneo hayo.