Shambulio la Urusi kwenye basi la abiria laua watu 9 Ukraine

Maafisa wa Ukraine wamesema shambulizi la droni la Urusi katika mkoa wake wa kaskazini wa Sumy limelenga basi la abiria mapema leo na kuua watu tisa na kuwajeruhi wengine wanne.

Maafisa hao wameongeza kwamba watu waliojeruhiwa wamepelekwa hospitalini huku wengine watatu wakiripotiwa kuwa katika hali mbaya. Chombo cha habari katika mji huo kimesema abiria katika basi hilo walikuwa wanahamishwa kutoka katika mji wa Bilopillia wakati shambulio lilipotokea.

Hayo yanajiri siku moja baada ya Moscow na Kyiv kufanya mazungumzo yao ya kwanza ya moja kwa moja ya amani huko Uturuki, baada ya miaka kadhaa ya kutofanikiwa kufikia makubaliano ya usitishaji mapigano. Licha ya vita kuendelea, Urusi na Ukraine ziliahidi hapo jana mjini Istanbul kuendelea na mchakato huo wa amani.
 

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *