Mauaji ya Kikatili, Paroko wa Kanisa Katoliki atekwa, auawa

Mauaji ya Kikatili, Paroko wa Kanisa Katoliki atekwa, auawa

Moshi/Nairobi. Nani wako nyuma ya mauaji haya? Jeshi la Polisi nchini Kenya, limeanzisha uchunguzi juu ya kutekwa na baadaye kuuawa kwa Paroko wa Parokia ya Igwamiti ya Kanisa Katoliki huko Nyahururi nchini Kenya, Padri John Maina.

Mitandao ya kijamii nchini Kenya, yanahusisha mauaji hayo na hatua ya Padre Maina kumkaribisha Makamu wa zamani wa Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua katika parokia hiyo, wakati wa maadhimisho ya Jubilee ya Parokia hiyo.

Kwa mujibu wa taarifa ya Polisi, imebainika Padri Maina alikuwa akifuatiliwa na baadhi ya watu waliokuwa wakimtaka awagawie pesa alizodaiwa kupewa baada ya kuongoza sherehe ya Jubilei ya miaka 25 ya Parokia ya Igwamiti, iliyohudhuriwa na Gachagua.

Taarifa ya Polisi iliyotolewa leo Mei 20, 2025 na Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Jinai (DCI) nchini Kenya, kupitia ukurasa wake wa X, imewataka raia wa Kenya kuwa watulivu kutokana na tetesi hizo mitandaoni.

DCI amebainisha Padre huyo alipatikana Mei 15, 2025 kando ya Barabara ya Nakuru akiwa na majeraha kichwani na alimweleza msamaria aliyemwokota kuwa alikuwa ametekwa katika Parokia yake, iliyopo umbali wa kilomita 40.

Ingawa taarifa hiyo ya DCI iliyowekwa katika akaunti rasmi ya DCI saa 1:13 ya usiku wa leo haikueleza ilipo gari yake aina ya Subaru Forester, lakini taarifa katika mitandao ya kijamii zinaeleza kuwa gari hilo bado halijapatikana hadi sasa.

Taarifa hiyo ya DCI imeeleza kuwa Aprili 27, 2025, Padri Maina alihudhuria Jubilei hiyo na ibada ya kuwekwa wakfu kwa Padri Simon Thuita iliyohudhuriwa pia na Gachagua, akiwa ameandamana na wanasiasa wengine wa Taifa hilo la Afrika Mashariki.

“Mnamo Mei 15, 2025, Padri Maina alipatikana kando ya barabara ya Nakuru kuelekea Nairobi na msamaria mwema, ambaye ni dereva wa bodaboda, karibu na kituo cha Diotomite akiwa na majeraha kichwani upande wa kushoto,”imeeleza sehemu ya taarifa hiyo.

“Dereva huyo alimpeleka Padri Maina katika Hospitali ya Misheni ya Mt. Joseph huko Gilgil. Alipofikishwa hospitalini, alionekana kuwa na majeraha ya wazi, yakiwemo ya kichwa upande wa kushoto yaliyokuwa yanavuja damu”.

“Licha ya jitihada za wahudumu wa afya, Padri Maina alifariki dunia akiwa anapatiwa matibabu dakika chache baada ya kulazwa,”ameeleza DCI.

“Mwili wake ulihamishiwa chumba cha kuhifadhia maiti katika Kaunti Ndogo ya Nyahururu kutokana na ombi la waumini wenzake kwa ajili ya kuhifadhiwa na kufanyiwa upasuaji wa uchunguzi kubaini sababu za kifo chake”

Kwa mujibu wa DCI, Mei 19, 2025, upasuaji ulifanywa na daktari wa serikali na matokeo ya awali yalionesha kuwa majeraha ya kichwani aliyokuwa nayo Padri Maina huenda hayakuwa chanzo cha kifo chake.

Mwanapalotholia wa Serikali, Titus Ngulungu ndiye aliyefanya uchunguzi wa mwili wa Padri huyo katika Hospitali ya Pope Benedict Catholic, lakini taarifa nyingine ambazo hazijathibitishwa zilidai alipigwa na kitu butu kichwani na wengine risasi.

Naibu Mkuu wa Dayosisi ya Nyahururu, Padri Timothy Maina pamoja na mapadri wengine 10 na ndugu wa marehemu walihudhuria uchunguzi huo, huku taarifa zingine zikidai mwili ulikuwa umejaa damu na majeraha yanayoonekana ni risasi.

“Hivyo, sampuli zilichukuliwa na kupelekwa kwa uchunguzi zaidi wa kimaabara wa sumu mwilini,”ameeleza DCI katika taarifa hiyo inayoshambuliwa mitandaoni.

DCI katika taarifa hiyo ameeleza kuwa maofisa wa upelelezi kutoka katika ofisi hiyo wanachunguza taarifa kwamba Padri Maina alikuwa amedai maisha yake yalikuwa hatarini, ingawa hakuwahi kuripoti hilo katika kituo chochote cha polisi.

Maofisa wa upelelezi wanaendelea kufuatilia ushahidi wa kitaalamu ili kuunda upya matukio ya mwisho ya Padri Maina na kuwakamata washukiwa, huku ikiwaomba wananchi wenye taarifa sahihi kuziwasilisha kwao.

“DCI inawahimiza wananchi kubaki watulivu katikati ya tetesi zinazozunguka mitandaoni. Timu yetu ya wachunguzi inafanya kazi kwa bidii na kwa uadilifu ili kulitatua suala hili kwa uangalifu wa hali ya juu, kuhakikisha haki inapatikana.”

Akizungumzia mauaji hayo, Seneta wa Nyandarua, John Methu ameelezea namna Padri huyo alivyompokea Gachagua na ujumbe wake katika maadhimisho ya Parokia ambayo yaliambatana na harambee kuchangia ununuzi wa gari.

“Tumeshtushwa sana kusikia kuhusu kifo cha Padri Maina. Padri alimuhudumia mheshimiwa Gachagua na timu yetu katika maadhimisho ya siku ya familia ya Parokia yaliyofanyika wiki mbili zilizopita. Apumzike kwa amani,”amesema.

Habari hii imeandikwa kwa msaada wa mitandao mbalimbali ya kijamii

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *