Yanga yatinga fainali FA, nne CAF hizi hapa

Timu ya Yanga imetinga hatua ya fainali ya michuano ya Kombe la Shirikisho (FA), baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0, dhidi ya maafande wa JKT Tanzania, katika mechi ya nusu fainali iliyopigwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga.

Ushindi huu wa Yanga unamaanisha kuwa sasa timu nne zinazoshiriki michuano ya CAF msimu ujao zimefahamika ambapo ni Simba na Yanga Ligi ya Mabingwa, huku Singida na Azam zikiwa kwenye Kombe la Shirikisho kwa kuwa timu itakayotwaa Kombe la FA ni kati ya zile nne bora za juu.

Katika mechi hiyo ya ushindani, ilishuhudia Yanga ikipata bao lililoipeleka fainali likifungwa na Prince Dube dakika ya 41, baada ya beki wa JKT Tanzania, Karim Mfaume kushindwa kuokoa mpira vizuri eneo la hatari na kumkuta mfungaji huyo.

Wakati timu hizo zikishambuliana kwa zamu, Yanga iliandika bao la pili lililofungwa na kiungo, Mudathir Yahya dakika ya 90, baada ya kupokea pasi safi iliyopigwa na Clatous Chama na kuuzamisha mpira wavuni uliomshinda kipa, Yakoub Suleiman.

Mechi hii ilikuwa ya kisasi kwa timu zote baada ya kushindwa kutambiana katika Ligi Kuu Bara mara ya mwisho zilipokutana Februari 10, 2025, na kutoka suhulu (0-0) ikiwa ni mechi ya kwanza kwa Kocha Mkuu wa Yanga, Miloud Hamdi kikosini humo.

Miloud aliyetangazwa na kikosi hicho Februari 4, 2025, akichukua nafasi ya Sead Ramovic aliyejiuzulu mwenyewe na baadaye kujiunga na CR Belouizdad ya Algeria, mechi hiyo ya JKT Tanzania ilikuwa ni ya kwanza akiwa na kikosi hicho msimu huu.

Yanga ilianza michuano hii ya FA hatua ya 64, kwa kuichapa Copco FC ya Mwanza mabao 5-0, kisha baada ya hapo ikakutana na Coastal Union hatua ya 32 na kuiondosha kwa kuifunga 3-1 na kutinga 16 bora na kuitoa Songea United ya Ruvuma mabao 2-0.

Katika hatua ya robo fainali, Yanga ikakutana na Stand United inayoshiriki Ligi ya Championship na kuichapa mabao 8-1, huku nyota wa timu hiyo, Stephane Aziz KI akifunga ‘Hat-Trick’, ikiwa ni ya kwanza msimu huu kwa mchezaji wa Ligi Kuu.

Kwa upande wa JKT ilianzia pia hatua ya 64 bora kwa kuitoa Igunga United ya Tabora kwa kuichapa mabao 5-1, kisha ikaitoa Biashara United inayoshiriki Ligi ya Championship kwa kuifunga 2-1, ikafuzu 16 bora na kuiondosha Mbeya Kwanza kwa 3-0.

Katika hatua ya robo fainali, kikosi hicho cha maafande kikafuzu na kwenda nusu fainali baada ya kutumia vyema Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo ambao ndio wa nyumbani kufuatia kuichapa Pamba Jiji FC inayoshiriki Ligi Kuu Bara kwa mabao 3-1.

Tangu michuano hiyo iliporejea tena msimu wa 2015-2016, Yanga ndio timu inayoongoza kwa kuchukua ubingwa huo mara nyingi zaidi, baada ya kufanya hivyo mara nne, ikifuatiwa na wapinzani wao wakubwa Simba, waliolichukua taji hilo mara tatu tu.

Kitendo cha Yanga kufuzu hatua ya fainali, kwa sasa inasubiri mshindi kati ya wapinzani wao wakubwa Simba itakayokuwa na kibarua kigumu cha kupambana na Singida Black Stars, katika nusu fainali ya pili ya michuano hii itakayopigwa Mei 31, 2025.

Mechi hiyo ya Simba na Singida itapigwa kwenye Uwanja wa Tanzanite Kwaraa uliopo Babati, Manyara, hivyo endapo kikosi hicho cha Msimbazi kitashinda kitakutana na Yanga katika fainali ya ‘Dabi ya Kariakoo’, itakayovuta hisia za mashabiki.

Yanga imefuzu fainali ya tano mfululizo ya michuano ya Kombe la Shirikisho (FA), tangu msimu wa 2020-2021, ambapo kati ya hizo imechukua ubingwa mara nne, huku ikikosa mara moja tu ilipochapwa na wapinzani wao Simba bao 1-0, msimu wa 2020-2021.

Tangu Yanga ikikumbane na kichapo hicho cha Simba, timu hiyo imechukua ubingwa wa michuano hiyo kwa mara tatu mfululizo, ikianza msimu wa 2021-2022, ilipoichapa Coastal Union kwa penalti 4-1, baada ya sare ya mabao 3-3, katika dakika 120.

Kwa misimu miwili mfululizo kuanzia 2022-2023 na 2023-2024, Yanga ikaichapa Azam FC bao 1-0, kisha ikashinda tena kwa mikwaju ya penalti 6-5, baada ya suluhu (0-0), mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex visiwani Zanzibar.

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *