Mtibwa bado pointi nne tu, ikiichapa Mbuni

Dar es Salaam. Mtibwa Sugar inahitaji pointi nne tu katika mechi zake nne ilizobakiza kwenye Ligi ya Championship baada ya leo kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 mbele ya Mbuni FC katika Uwanja wa Manungui Complex, Morogoro.

Mabao ya Mtibwa Sugar leo yamepachikwa na Erick Kyaruzi na Omary Marungu huku lile la Mbuni likipachikwa na Thomas Malulu.

Matokeo hayo yameifanya Mtibwa Sugar kufikisha pointi 63 na hivyo kuifanya ihitaji pointi nne ili ifkishe pointi 67 ambazo zitaihakikishia kumaliza katika nafasi mbili za juu kwenye msimamo wa Championship ili ipande Ligi Kuu msimu ujao.

Upo pia uwezekano kwa Mtibwa Sugar kupanda Ligi Kuu ikiwa itashinda mchezo unaofuata dhidi ya Mbeya Kwanza na timu za Stand United na Geita Gold zikashindwa kupata ushindi katika mechi zao.

Katika raundi inayofuata, Geita Gold itakuwa nyumbani kuikaribisha Songea United huku Stand United yenyewe ikiikaribisha Green Warriors.

Kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi Pwani, wenyeji Green Warriors waliibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Geita Gold, matokeo ambayo hapana shaka yamepokelewa kwa furaha na Mtibwa Sugar, Mbeya City na Stand United ambazo zipo kileleni mwa msimamo wa ligi.

Kichapo hicho cha leo kutoka kwa Green Warriors kimeifanya Geita Gold kubaki katika nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ya Championship ikiwa na pointi zake 51, ikizidiwa kwa pointi 12 na Mtibwa Sugar inayoongoza, ikiachwa kwa pointi tano na Mbeya City iliyo nafasi ya pili ikiwa na pointi 56 na imeachwa kwa pointi nne na Stand United yenye pointi 55 ikiwa nafasi ya tatu.

Green Warriors kwa kuifunga Geita Gold leo, imepanda kwa nafasi moja hadi nafasi ya 11 kwenye msimamo wa ligi ikifikisha pointi 23.

Vita ya kupanda ilipofikia na mechi zilizobaki kwa timu nne za juu

MTIBWA SUGAR-Pointi 63

-Mbeya Kwanza vs Mtibwa

-Bigman vs Mtibwa Sugar

Transit Camp vs Mtibwa Sugar

Mtibwa Sugar vs Kiluvya United

MBEYA CITY-Pointi 56

Polisi Tanzania vs Mbeya City

Geita Gold vs Mbeya City

Mbeya City vs Cosmopolitan

Mbeya City vs Green Warriors

STAND UNITED- Pointi 55

Stand United vs Green Warriors

Cosmopolitan vs Stand United

Polisi Tanzania vs Stand United

Stand United vs Geita Gold

GEITA GOLD- Pointi 51

Geita Gold vs Songea United

Geita Gold vs Mbeya City

Biashara United vs Geita Gold

Stand United vs Geita Gold

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *